
WATU 13 wamefariki na mamia kujeruhiwa baada ya tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 6.5 kukumba nchi za Afghanistan na Pakistani, huku mitetemeko ikisikika hadi mji mkuu wa India New Delhi.
Kaskazini Magharibi mwa Pakistan, takriban watu tisa waliuawa na 44 kujeruhiwa, afisa wa serikali amesema leo Machi 22, 2023. Hospitali katika jimbo la kaskazini la Khyber Pakhtunkhwa ziliwekwa katika hali ya hatari usiku kucha.
Nchini Afghanistan, takriban watu wanne waliuawa na 50 kujeruhiwa, afisa wa wizara ya afya aliliambia shirika la habari la Reuters.
Kitovu cha tetemeko la ardhi kilikuwa kilomita 40 (maili 25) kusini mashariki mwa mji wa Afghanistan wa Jurm, karibu na mipaka ya Pakistan na Tajikistan, Utafiti wa Jiolojia wa Marekani (USGS) ulisema jana.
Tetemeko hilo lilisikika katika eneo lenye upana wa zaidi ya kilomita 1,000 (maili 621) na takriban watu milioni 285 nchini Pakistan, India, Uzbekistan, Tajikistan, Kazakhstan, Kyrgyzstan, Afghanistan na Turkmenistan, Kituo cha Ulaya-Mediterranean Seismological Center kilisema.