Biashara

BoT yaonesha ukusanyaji mzuri wa mapato Januari

RIPOTI ya tathmini ya uchumi ya kila mwezi ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa mwezi Februari imebainisha kuwa ukusanyaji wa mapato katika mwezi Januari mwaka huu yalikuwa ndani ya malengo ya serikali.

Katika ripoti hiyo ambayo ipo katika tovuti ya BoT, inaonesha kuwa jumla ya mapato ya ndani yanayojumuisha makusanyo ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa yalifikia Sh bilioni 2,207.8.

Kwa mujibu wa BoT, mapato ya Serikali Kuu katika kipindi hicho yalikuwa Sh bilioni 2,120.8 ambapo makusanyo ya kodi yalikuwa Sh bilioni 1,830.7 sawa na asilimia 103.6 ya lengo la mwezi huo.

Mafanikio hayo ya ukusanyaji wa mapato kwa mujibu wa BoT yalichangiwa na kuongezeka kwa uagizaji wa bidhaa kutoka nje hususani bidhaa zinazotumika kama malighafi za kuzalisha bidhaa nyingine au bidhaa za mwisho pamoja na mapato yanayohusiana na juhudi zinazoendelea za kufufua shughuli za kiuchumi na shguhuli za usimamizi wa kodi.

Kwa upande wa Serikali za Mitaa, makusanyo yalikuwa Sh bilioni 87 ambapo misaada ilikuwa Sh bilioni 1.3. Wakati akiwasilisha bungeni Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka wa fedha 2022/23 Juni 14 mwaka jana, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba, aliliomba Bunge liidhinishe Sh trilioni 41.48 kwa ajili ya matumizi ya maendeleo na kawaida kwa mwaka wa fedha 2022/23.

Dk Mwigulu alisema kwa mwaka huu wa fedha Sh trilioni 41.48 zinatarajiwa kukusanywa na kutumika huku mapato ya ndani yakitarajiwa kuwa Sh trilioni 28.02, sawa na asilimia 67.5 ya bajeti yote.

Related Articles

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button