
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana katika mwaka wa fedha wa 2022/23 mikopo yenye thamani ya Sh bilioni 1.88 imetolewa kwa miradi 85 ya vijana.
Akizungumza leo Machi 12, 2023 Jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa upokeaji wa maombi kwa ajili ya programu endelevu ya uwezeshaji, Waziri Majaliwa amesema serikali imeendelea kutumia mifuko ya kukopesha vijana ili kurahisisha upatikanaji wa mikopo na mitaji.
Katika kuhakikisha vijana hao wananufaika na mikopo hiyo, Waziri Majaliwa amesema serikali imezielekeza halmashauri zote nchini kutenga maeneo kwa ajili ya kufanyia shughuli za uzalishaji mali ambapo ekari 274,091 zimetengwa kwa ajili ya shughuli za Kilimo na uendelezaji viwanda vidogo vidogo.
“Aidha, mita za mraba 434,642 zimetengwa kwaajili ya shughuli za biashara na zaidi ya vijana 194,553 wamefaidika, Halmashauri endeleeni kutenga maeneo kwa ajili ya ufanyaji biashara”. Amesema Waziri Majaliwa.